JOYCE BANDA AKUBALI YAISHE, AMUOMBA RADHI MUTHARIKA

 

Kiongozi wa upinzani nchini Malawi, Peter Mutharika, ametangazwa kuwa mshindi wa kiti cha urais katika uchaguzi wa Mei 20 baada ya Mahakama Kuu nchini humo kuruhusu utoaji wa matokeo.

Tume ya uchaguzi nchini humo imemtangaza bwana Mutharika, ambaye ni kiongozi wa chama cha Democratic Progressive Party (DPP), kuwa ameshinda kwa asilimia 36.4.

Mgombea wa chama cha kihafidhina, Lazarus Chakwera, ameshika nafasi ya pili akiwa na asilimia 27.8 ya kura huku Rais anayeondoka madarakani Joyce Banda akishika nafasi ya tatu kwa asilimia 20.2.

Matokeo hayo yametangazwa muda mfupi baada ya mahakama kuu kutupilia mbali ombi la kutaka kucheleweshwa kwa utoaji wa matokeo ya uchaguzi huo. Mahakama hiyo pia ilikataa ombi la kutaka kura zihesabiwe upya kwa mikono pamoja na wito wa kutaka uchaguzi huo urudiwe.

Kabla ya uamuzi huo wa mahakama, mtu mmoja alipoteza maisha kusini mashariki mwa mji wa Mangochi baada ya polisi kufyatua gesi ya kutoa machozi na risasi za mpira dhidi ya waandamanaji waliokuwa wakitaka kura zihesabiwe upya.

Wito wa kutaka kura zihesabiwe upya ulianza kutolewa na chama cha Malawi Congress Party (MCP) cha rais wa zamani wa nchi hiyo Kamuzu Banda baada ya matokeo ya awali kuonesha mgombea wao, Chakwera, akiwa katika nafasi ya pili.

Aidha, Rais Banda alikuwa ametangaza kufuta matokeo ya uchaguzi na kutangaza kurudiwa kwa uchaguzi kwa madai kuwa tume ya uchaguzi ilikuwa imegubikwa na kasoro nyingi ikiwemo kushindwa kukagua rajisi ya wapiga kura katika baadhi ya vituo vya kupigia kura.

Hata hivyo, mahakama kuu ilifutilia mbali uamuzi wa Banda ikisema kuwa rais hana mamlaka ya kubatilisha uchaguzi.


Wakati hayo yakijiri, taarifa zilizoifikia Mzizima24 hivi punde zinasema kuwa Bi Joyce Banda amemtaka radhi bwana Peter Mutharika na kumuomba nafasi ya kujiunga na chama chake cha DPP baada ya kutangaza kukivunja chama chake.
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment