VIPODOZI KUANGAMIZA MAMIA YA WANAWAKE

 

Idadi ya wanawake wanaoota ndevu mithili ya wanaume inazidi kuongezeka nchini. Hali hiyo imewashtua pia wataalamu wa afya, ambao wamesema ingawa hakuna takwimu halisi ya wenye tatizo hilo, lakini hali inatisha.

Uchunguzi uliofanywa kuhusiana na suala hilo umebaini kuwa hali hiyo inasababishwa na mambo mbalimbali, yakiwemo ya kurithi, utumiaji mbaya wa vyakula na matumizi holela ya vipodozi.

Daktari Adam Nyalandu kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), alisema kuwa tatizo la wanawake tatizo la wanawake kuota ndevu linatokana na sababu nyingi ikiwemo matumizi ya vipodozi vyenye kemikali na vyakula vya kusindika.

Alisema matumizi ya vipodozi vya aina tofauti vyenye viambata vya sumu vimekuwa vikichangia madhara mbalimbali kwa wanawake ikiwemo uotaji wa ndevu.

Pia alisema baadhi ya wanawake wamekuwa wakitumia vipodozi vya aina tofauti ili kutakatisha ngozi zao zionekane kama za wazungu bila kujua madhara yake. Alisema vipodozi vingi vina viambata vyenye sumu ambayo ni tishio kiafya.

Dk. Nyalandu alifafanua kuwa baadhi ya vyakula vya kusindika vimekuwa vikitengenezwa kwa kutumia kemikali nyingi ambazo zinachangia tatizo hilo kwa wanawake, ambapo madhara yake kwao yameanza kuonekana waziwazi.

“Mfano ulikuwa huli nyama za kopo au vyakula vya kusindika ambavyo kemikali inatumika kuvisindika sasa unakula, vinaweza kusababisha hilo tatizo kwa kiwango kikubwa,” alisema Dk. Nyalandu.

Alisema ni vema wanawake wakawa makini na vipodozi wanavyotumia kwa kuchunguza viambata vya sumu ili kuepuka kuvitumia kwa usalama wa fanya zao.

Kwa upande wake, Dk. Abdallah Mandai aliwaonya wanawake na kuwataka kuachana na matumizi ya vipodozi vyenye kemikali sanjari na ulaji wa vyakula vya kizungu.

Alisema wanawake wengi, hususan wa mijini, wamekuwa wakitumia vipodozi vyenye kemikali huku wakila vyakula vinavyoandaliwa kisasa zaidi vikiwa na mafuta mengi au kukaangwa na hivyo kuharibu homoni zao na kusababisha madhara mbalimbali.

Dk. Mandai alisema matumiz ya vipodozi sit u yana athari ya kuwafanya wanawake waote ndevu, bali wengi wao wanaopata ujauzito hujifungua kwa njia ya upasuaji.

“Dawa ya nywele wanayotumia pamoja na vipodozi vyenye kemikali huchangia kwa kiasi kikubwa kuota ndevu. Katika hili la vipozozi tambua kuwa chochote kinachokuwa juu ya ngozi ya binadamu kina uwezo wa kusambaa mwilini na kusababisha madhara mbalimbali,” alisema Dk. Mandai.

Akitolea mfano, alisema zamani wanawake, wakiwemo wajawazito, walikuwa wanakula vyakula vya asili na kwamba walizuiwa hata kula mayai, hali iliyokuwa ikiwasaidia wengi wao kujifungu kwa njia ya kawaida.

“Kuna wakati wajawazito 10 wanakuwa wamelazwa hospitali, kati yao pengine wawili tu ndiyo wanaweza kujifungua kwa njia ya kawaida… wengine wanafanyiwa upasuaji,” alisema.

Aliongeza kuwa tatizo hilo linaweza kupungua kwa kiasi kikubwa iwapo wanawake watabadilika na kupenda vitu vya asili na kuacha kuiga utamaduni wa kimagharibi ambao una athari kubwa kwao.

“Ushauri wangu ni kwamba tuache kupeperusha bendera ya umagharibi (kuiga tamaduni za kigeni), tudumishe mila zetu ikiwemo kula vyakula vya asili, matatizo haya yatapungua kwa kiasi kikubwa,” alisema Dk. Mandai.

Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Gaudensia Simwanza alinukuliwa wakati mmoja akisema mamlaka hiyo imepiga marufuku vipodozi vyote vyenye viambata sumu, lakini watu wanaendelea kuvitumia.

“Madhara yake ni makubwa, mwanamke mjamzito ni rahisi kuzaa mtoto tahira au mimba ikatoka,” alisema huku daktari wa magonjwa ya ngozi wa kituo cha Afya Centre, Isaack Maro akisema wanawake wanaotumia vipodozi vyenye viambata sumu huathirika kwa kiasi kikubwa bila kujijua.

Alisema madini ya zebaki yanayotumika katika vipodozi vingi hayatoki kwa urahisi mwili kwani hujazana mwilini kwa muda mrefu na kusababisha maradhi.

“Watu wanaotumia vipodozi hivyo, figo zao huwa zimetoboka kutokana na kuharibiwa na madini hayo,” alisema Dk. Maro.

CHANZO: Jambo Leo Septemba 23,2013
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment