TUKIO LA NAIROBI: USALAMA WA TAIFA WA KENYA KUFUMULIWA?

Kenya has begun three days of national mourning following the end of the four-day standoff at Nairobi 



KUTOKANA na shambulio lililofanywa na kundi la Al Shabaab walioteka jumba la biashara la Westgate na kuua makumi ya raia nchini Kenya, serikali ya nchi hiyo inakusudia kufumua Idara ya Usalama wa Taifa (NIC).

Sababu za serikali kuchukua hatua hiyo ni madai kwamba imeshindwa kuzuia tukio hilo, huku ikihangaika na watu wadogo wadogo wasio tishio kwa usalama wa nchi.

Akizungumza katika Bunge lililoitishwa kwa dharura jana jijini Nairobi, Naibu Rais, William Ruto, alisema washambualiaji hao wamefanikiwa kufanya unyama huo kwa sababu idara hiyo ilikosa umakini.

Ruto alisema lazima idara hiyo ifumuliwe na kufanyiwa mabadiliko makubwa. Alieleza mshangao wake wa namna watu hao walivyofanikiwa kupenya na kufanya mauaji makubwa wakati taifa linatumia fedha nyingi katika sekta ya usalama.

“Tumekuwa tukitumia fedha nyingi kwa ajili ya vikosi vya usalama nchini hapa, lakini maofisa wetu wamekuwa hawafanyi kazi ipasavyo, zaidi ya kubaki wakikimbizana na matatuu ‘daladala’ na mama ntilie,” alisema.

Katika mapambano hayo wapiganaji tisa wa kundi la Al Shabaab wameuawa, huku askari sita wa jeshi wakipoteza maisha na wengine wanane wakijeruhiwa. Wabunge wengi walisema tukio hilo limedhihirisha kushindwa kwa idara hiyo.

Mbunge wa Lagdera, Mohammed Shidiye, alisema: “Nafikiri kwamba huu ni wakati mwafaka wa kufanya upasuaji wa idara hii ili tuweze kupata watu wachapakazi.”

Mbunge wa Westland, Tim Wanyonyi, alidai wafanyakazi wengi wa idara hiyo wamekuwa wakisinzia katika kazi zao na kusababisha kushindwa kuhakikisha Wakenya wanakuwa salama.

Mashambulizi hayo yanadaiwa kuwahusisha watu wawili wanaodaiwa kuwa raia wa Marekani wenye umri wa miaka 18 na 19, wakiwa na asili ya Kisomali, wanaosadikiwa kuishi mjini Minnesota, na mmoja wa Uingereza, anayedaiwa kuhusika na matukio mengi ya kigaidi.

Shutuma hizo za serikali na wabunge zinatokana na kuwapo kwa taarifa kwamba, washambualiaji hao wamekuwa wakidai kuwa watazishambulia nchi zote za Afrika zitakazothubutu kupeleka majeshi yake Somalia kuisaidia serikali ya nchi hiyo.

Taarifa zinasema waliovamia jengo hilo ni sehemu ya wanamgambo hao, na kwamba huenda ndio waliohusika na mashambulizi kadhaa yaliyotokea katika nchi ya Uganda miaka kadhaa iliyopita.

Shambulio la juzi katika jengo la Westgate mjini Nairobi limegharimu roho za zaidi ya watu 62 kutoka mataifa mbalimbali, huku watu wengine zaidi ya 170 wakijeuhiwa na wengine zaidi ya 50 wakiwa hawajulikani waliko.

Kundi hilo linadaiwa kufanya shambulio hilo kulipa kisasi dhidi ya Kenya kutokana na uamuzi wa nchi hiyo kupeleka jeshi lake Somalia mwaka 2011 kuwafurusha wapiganaji hao wa Al Shabaab waliokuwa wakishikilia sehemu kubwa ya nchi hiyo.

Katika shambulio la nchini Uganda, kundi la Al Shabaab lenye mafungamano na Al-Qaeda lilidai kufanya shambulio la mabomu mawili ya kujitoa mhanga mjini Kampala na kuua watu 74 waliokuwa wakiangalia mechi ya mpira wa miguu ya Kombe la Dunia, Julai 2010.

Wachambuzi wa masuala ya usalama wanasema kuwa kundi hilo linaweza kuishambulia nchi yoyote na wakati wowote, likiona masilahi yake yanatishiwa.

“Tuliwaonya Uganda wasipeleke majeshi yao Somalia lakini wakatupuuza. Tuliwaonya kuacha kuwaua watu wetu, na hilo walilipuuza pia. Mashambulizi ya Kampala yalikuwa ni ujumbe mdogo tu kwao, tutawalenga na kuwashambulia mahali popote ikiwa Uganda haitaondoa majeshi yake nchini mwetu,” alisema msemaji wa Al Shabaab, Ali Mahamud Rage.

Rage pia aliionya Burundi kuwa ingekuwa nchi inayofuata katika mkakati wa mashambulizi wa kundi hilo kutokana na kitendo chake cha kupeleka majeshi yake nchini Somalia.

Itakumbukwa shambulio la Jumamosi si la kwanza kwa nchi za Afrika Mashariki. Mwaka 1998 balozi za Marekani hapa nchini na Nairobi, Kenya zilishambuliwa na  al-Qaida na kuua watu 224 raia wa nchi hizi mbili na Wamarekani 12.

Vilevile mwaka 2002, al-Qaida waliishambulia kwa makombora ndege ya shirika la ndege la Israel na hoteli inayomilikiwa na raia wa nchi hiyo iliyopo mjini Mombasa.

Kwa muda mrefu wachambuzi wamekuwa na woga kuwa kundi la al Shabaab lilikuwa likipata nguvu na kugeuka kuwa kitisho cha amani kwa nchi zote za Afrika Mashariki na za Pembe ya Afrika. Taasisi ya kimataifa ya utafiti na uzuiaji migogoro ya International Crisis Group iliwahi kusema kuwa:

“Kama ushawishi wa wapiganaji wa nje ukikua na kupata nguvu ndani ya kundi la al Shabaab, basi mabadiliko ya haraka ya kundi hilo kuwa tawi kamili la al-Qaida itakuwa haizuiliki tena. Kwamba kundi hilo litasababisha matatizo makubwa hata nje ya mipaka ya Somalia, na jumuiya ya kimataifa haiwezi kuchagua kubaki kuwa watazamaji tu.”


Tayari serikali ya Tanzania imesema kuwa imejiimarisha vema kutokana na tishio hilo, huku Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai nchini, Robert Manumba akidai vikosi vya ulinzi na usalama viko kamili.

CHANZO: Tanzania Daima
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment