Mabingwa wa soka wa Tanzania Bara, Yanga wanaweza
kumkosa mshambuliaji wao mahiri Mrisho Ngassa baada ya klabu moja ya Qatar
kuonyesha nia ya kumsajili huku mchezaji huyo akikiri kwamba dau walilomuahidi linamshawishi.
Habari za uhakika ambazo Mwananchi ilizipata jana
zilisema kuwa, tayari Ngassa amekwishafanya mazungumzo na klabu hiyo ambayo ipo
tayari kuilipa Simba SC milioni 45 anazodaiwa na kuifidia Yanga kwa kumuuza
mchezaji huyo.
Taarifa hizo zimesema kuwa klabu hiyo inataka kumtumia
Ngassa baada ya usajili wa dirisha dogo.Ngassa alithibitisha hilo huku akikataa
kutaja jina la timu hiyo kwa sababu za kisheria za usajili wa wachezaji na
kuogopa adhabu ya Shirikisho la Soka Kimataifa (Fifa).
Mchezaji huyo alikiri kuwa timu hiyo ipo tayari kumpa
mkataba wa miaka miwili na kuzilipa Simba SC na timu yake ya sasa, Yanga.
Alisema kuwa hatua hiyo imekuja baada ya kuona suala
lake la kuitumikia Yanga katika Ligi Kuu ya Tanzania Bara linashika sura mpya
kutokana na mvutano wa malipo.
Alifafanua kuwa klabu hiyo imemuahidi donge nono na
kuamua kufuta msimamo wake wa zamani wa kutaka kucheza soka hapa nchini
kutokana na maslahi anayopata.
“Maslahi yao mazuri na mazingira waliyoniahidi
kimkataba, nimevutiwa nao kutokana na ukweli kuwa suala langu la kuichezea
Yanga limekumbwa na vipingamizi vingi,” alisema Ngassa.
Alisema kuwa baadhi ya wadau wa Yanga na marafiki zake
wana nia njema ya kutaka kumlipia fedha anazodaiwa na Simba, lakini uongozi wa
Yanga bado haujatoa jibu la sakata hilo.
“Nimemaliza kifungo cha mechi sita, sasa suala
lililobaki ni malipo, viongozi hawajatoa jibu mpaka sasa, ” alisema Ngassa.
Makamu Mwenyekiti wa klabu ya Yanga, Clement Sanga
alikiri kuwa bado hawajailipa Simba fedha wanazomdai Ngassa kutokana na
majadiliano waliyokuwa nayo.
Sanga alisema kuwa wana uhakika kuwa Ngassa ambaye
anafanya mazoezi ya nguvu na Yanga, atacheza Jumamosi dhidi ya timu ngumu ya
Ruvu Shooting.
CHANZO: Mwananchi
0 comments:
Post a Comment