MCHUNGAJI Ambilikile Mwaisapila wa Kanisa la Kiinjili la
Kilutheri Tanzania (KKKT) amesema Mungu ameendelea kujifunua kwake na
kumuonyesha kuwa Tanzania itakuwa kioo cha Afrika na baadaye kioo cha dunia.
Alitoa kauli hiyo juzi mbele ya Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda wakati msafara wake uliposimama katika Kijiji cha Samunge, wilayani
Ngorongoro, ambako alikwenda kumsalimia nyumbani kwake pamoja na kuzungumza na
wananchi akiwa njiani kurejea mjini Arusha.
Mchungaji Mwaisapila maarufu kama ‘Babu wa loliondo’
alisema kuna mambo mengi ambayo yameandikwa kwenye Biblia, lakini hayakutokea
Israeli na sasa yatafanyika Samunge. “Mungu ametupenda sana, yanakuja mambo
makubwa na wala hayako mbali. Kama mimi ni mzee na nitayaona, kwa hiyo mtarajie
kuwa hayako mbali kutokea,” alisema huku akishangiliwa.
Alisema katika mafunuo aliyopewa na Mungu, ameonyeshwa
kwamba watu wengi zaidi watafurika kijijini Samunge kuliko ilivyokuwa awali.
Alitumia fursa hiyo kuishukuru serikali kwa misaada
iliyotoa wakati wa ‘kugawa kikombe’ ikiwemo mahema, maji na ulinzi.
Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Arusha kwa ziara maalumu
ya kusikiliza matatizo ya ardhi yanayowakabili wakazi wa Wilaya ya Ngorongoro,
katika tarafa za Ngorongoro, Loliondo na Sale alisema anakubaliana na utabiri
wa Mchungaji Mwaisapila kwani Tanzania imejaliwa gesi nyingi na mafuta mengi
ambavyo vitabadili sura ya taifa.
“Mungu ametupa gesi nyingi, katika miaka miwili tutakuwa
na umeme kila mahali. Tuna makaa ya mawe ambayo ni nishati kubwa na sasa tuna
fursa ya kupata nishati ya umeme kutoka ardhini (geo-thermal) katika Ziwa
Natron,” alisema.
Alisema Tanzania imekuwa kimbilio la kila mwekezaji na
sababu kubwa ni amani na utulivu uliopo nchini.
CHANZO: Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment