Ugonjwa hatari wa mahindi waingia nchini





Ugonjwa hatari unaoshambulia mahindi na kusababisha saratani kwa binadamu umeingia nchini na wakulima sasa wametahadharishwa kutokula mahindi hayo wala unga ambao haujakobolewa.
Mahindi yaliyoathiriwa na ugonjwa huo huota ‘fungus’ ambao ina sumu inayoitwa ‘Aflatoxin’ ambayo inaweza kusababisha madhara kwa wanyama na binadamu hususan ugonjwa wa saratani.
Mbali na kutikisa mikoa kadhaa na kusababisha hasara kubwa kwa wakulima, ugonjwa huo ambao umeanzia nchini Kenya unaendelea kusambaa kwa kasi na sasa umeingia pia nchini Uganda.
Awali ugonjwa huo uliripotiwa kuzikumba wilaya za Babati mkoani Manyara na Meatu mkoani Shinyanga tu, lakini sasa umesambaa hadi katika mikoa jirani ikiwamo Kilimanjaro.
Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro, Leonidas Gama jana alilithibitishia gazeti hili kuwa mkoa wake umekumbwa na ugonjwa huo na tayari umesambaa katika wilaya tatu; Moshi Vijijini, Siha na Hai. “Ni kweli baadhi ya wilaya zimekumbwa na ugonjwa huo, bahati mbaya sana hauna tiba na unasambaa kwa kasi... Wataalamu wanaendelea kuwaelimisha wakulima kutambua dalili zake,” alisema Gama.
Gama alisema endapo mkulima atabaini shamba lake kushambuliwa na ugonjwa huo katika hatua za awali, anachotakiwa kufanya ni kung’oa mimea yote ya mahindi na kuichoma moto.
Mkuu wa Wilaya ya Hai, Novatus Makunga alisema takriban hekari 14 zimeshambuliwa na ugonjwa huo katika shamba la Watawa wa Kanisa Katoliki Mailisita na shamba la mkulima wa Lambo.
Alisema tayari wataalamu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya Selian (SARI) ya Jijini Arusha wamefika wilayani humo na kutoa tahadhari kwa wakulima juu ya athari za ugonjwa huo. Mfanyabiashara mashuhuri wa mjini Moshi, John Bennett anayemiliki mgahawa wa Golden Shower aliitaka Serikali kutoa elimu kwa wananchi na wafanyabiashara na kuchukua tahadhari.
“Utajuaje unga wa dona haukutokana na hayo mahindi au pumba ya chakula cha mifugo hayakutokana na hayo? Hili jambo ni zito sana si la kufanyia utani hata kidogo”alisema Bennett.
Mkulima wa Kijiji cha Kikavu Chini wilayani Hai, Justine Mvungi alisema wataalamu kutoka SARI wamewataka kuchoma moto miche ya mahindi ambayo watagundua imeshambuliwa.
“Wametuambia takriban shamba likishambuliwa, tung’oe mahindi hayo na kuyachoma moto, wametuambia kama tulishavuna basi tukoboe mahindi hayo maana kiini chake kina madhara,”alisema.
“Aliongeza kusema” hata tukikoboa mahindi tumeambiwa zile pumba zake tusiipe mifugo kwa sababu itaathirika… Ugonjwa huu wa mmea wa mahindi umeleta taharuki kubwa kwa wakulima na wananchi.”
Mkulima huyo alisema kwa mujibu wa watalaamu hao, kiini hicho kina madhara kwa binadamu na huweza kusababisha ugonjwa wa saratani ya koo na pia kusababisha matatizo katika njia ya chakula.
Mtaalamu Bingwa wa Kilimo Wilaya ya Moshi Vijijini, Dk Estomih Masha alisema ingawa haijathibitika kitaalamu athari kwa binadamu, kuna uwezekano mkubwa wa kuwapo madhara. “Kama mahindi yanaota ‘fungus’ ambao wanatoa sumu inayoitwa ‘Aflatoxin’ hiyo inaweza kuleta aina fulani ya ‘cancer’ (saratani), hivyo jamii ni lazima ichukue tahadhari kubwa,” alisema Dk Masha.
Ofisa Kilimo kutoka Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kutoka kitengo cha afya ya mimea, Katemani Mdili alikaririwa akisema ugonjwa huo unasababishwa na virusi vya aina mbili. “Changamoto kubwa tuliyonayo ni kwamba hadi sasa hakuna viuatilifu vya kuudhibiti ugonjwa huu na husambazwa kwa kasi na wadudu aina ya Aphids na Thrips,” alikaririwa Mdili.
Alisema dalili za ugonjwa huo ni majani ya juu ya mahindi kugeuka kuwa rangi ya njano na hatimaye kukauka kuanzia pembezoni mwa jani kwenda katikati na kisha mmea kufa.
Alisema ugonjwa huo hatari unajulikana kitaalamu kama Maize Lethal Necrosis Disease (MLND) na hutokea wakati virusi vya aina mbili vinapoathiri mmea wa mahindi kwa pamoja. Virusi hivyo ni Maize Chlorotic Mottle Virus (MCMV) na Sugar Cane Mosaic Virus (SCMV) na tayari Shirika la Chakula Duniani (FAO) limethibitisha kuwapo kwa ugonjwa huo.

CHANZO: Mwananchi
Share on Google Plus

About mahamoud

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment