BAJETI YA MAJI YAKWAMA




SPIKA wa Bunge Anne Makinda amelazimika kuahirisha shughuli za Bunge mpaka jumatatu kwa lengo la kuinusuru Bajeti ya wizara ya maji baada ya kuibuka malumbano makali baina ya serikali na wabunge huku wengi wao wakionyesha dalili za wazi za kuipinga bajeti hiyo.

Sanjari na uamuzi huo Spika Makinda ameiagiza kamati ya Bajeti,kamati ya sekta na Serikali kutafuta ufumbuzi wa nini kifanyike kabla ya kuruhusu mjadala huo urudishwe Bungeni wiki ijayo kwa ajili ya majadiliano kabla ya kupitishwa na wabunge.

Spika Makinda anasema suala la maji linawagusa watanzania kwa asilimia mia katika maisha yao ya kila siku na kwamba kuendelea kujadili jambo linalopingwa na kila mbunge anayesimama bila kujali itikadi za kisiasa Bunge litakuwa halitendi haki kwa jamii.

Awali Waziri Mkuu Mizengo Pinda ameliambia Bunge kuwa kutokana na ufinyu wa bajeti ya maji kwa mwaka huu wa fedha serikali itatoa kipaumbele kwa maeneo ya vijijini ambayo yanadaiwa kuwa katika hali mbaya ya upatikanaji wa huduma hiyo.

Waziri Mkuu Pinda ametoa kauli hiyo kufuatia swali la Kiongozi wa kambi ya upinzani Bungeni Freeman Mbowe wakati wa maswali na majibu ya papo hapo ambayo huulizwa kwake na wabunge kila siku ya alhamisi.

Katika swali lake Mbowe alitaka kujua ni kwanini serikali isitoe kipaumbele kwenye suala la uvunaji wa maji akiamini kuwa hatua hiyo inaweza kuwa suluhu mbadala ya kuondokana na kero ya maji nchini.
Wakichangia makadirio ya mapato na matumizi kwa wizara ya maji baadhi ya wabunge wameitaka Serikali kutafuta njia mbadala ya kumaliza changamoto ya huduma hiyo ambayo inadaiwa kutishia usalama wa maisha kwa baadhi ya wanawake waishio vijijini ambapo wengi wao hukumbana na wanyama hatari na hata nyoka nyakati za usiku.

Mapema jumatano hii akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake waziri wa maji Profesa Jumanne Maghembe amesema changamoto kubwa inayoikabili sekta hiyo ni ongezeko la watu,ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii pamoja na hujuma katika miundo mbinu ya maji inayofanywa na baadhi ya watu wanaojihusisha na biashara ya vyuma chakavu.

Wizara hiyo imeomba kuidhinishiwa jumla ya shilingi bilioni 398.3 ambapo bilioni 18.9 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi na bilioni 379.4 ni fedha za maendeleo ingawa tarakimu hizo zinaweza kubadilika wakati wowote kuanzia sasa baada ya majadiliano kati ya kamati hizo mbili na serikali.

CHANZO: Star tv
Share on Google Plus

About mahamoud

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment