| Rais wa Palestina Mahmoud Abbas akizungumza kwenye mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa (picha ya maktaba) |
Mamlaka ya Palestina imesema kuwa itaendelea na juhudi
zake katika Umoja wa Mataifa za kutaka kutambuliwa rasmi kama taifa licha ya
juhudi za pamoja za Marekani na Israel kukwamisha jaribio hilo.
Wapalestina watawasilisha azimio hilo leo katika Baraza
la Usalama la Umoja wa Mataifa huku kukiwa na taarifa kuwa Washington na Tel
Aviv zinatengeneza upinzani wa pamoja dhidi ya hatua hiyo, ambapo Marekani
imekuwa ikitumia kura ya turufu kuzuia azimio lolote lisiloupendelea utawala wa
Israel.
Hata hivyo, maafisa wa Kipalestina wanaonekana kutojali,
wakisema kuwa watawasilisha azimio hilo ambalo linataka kuwekwe muda wa mwisho
wa miaka miwili kwa Israeli kuondoa majeshi yake katika ardhi za Palestina
inazozikalia kwa mabavu.
“Tutawasilisha muswada wetu kesho mbele ya Baraza la
Usalama”, alisema mshauri wa Rais wa Palesina Mahmud Abbas hapo jana.
Aidha, Mwakilishi mkuu wa Palestina kwenye mazungumzo ya
amani Saeb Erakat alitoa maelezo kama hayo wakati wa mazungumzo baina yake na
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani, John Kerry, mjini London, ambapo
mwanadiplomasia huyo wa Marekani alionya kuwa serikali yake itazuia azimio
lolote linalodai uhuru wa Palestina.
Kerry ameripotiwa kufanya mazungumzo kwa siku tatu na
baadhi ya nchi za Ulaya katika jaribio la kuizima hoja hiyo.
Wakati huo huo Erakat alionya kuwa hatua ya Marekani
kutumia kura ya veto itawafanya Wapalestina kuomba uanachama wa taasisi kadhaa
za kimataifa ikiwemo Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC), ambapo
watakuwa na uwezo wa kuushtaki utawala wa Israeli kwa uhalifu na jinai za
kivita.
Marekani pia inapinga juhudi ya Palestina kupata
uanachama wa Mahakama ya ICC.
Kwa miezi kadhaa sasa, Serikali ya Umoja wa Kitaifa ya
Palestina imekuwa ikitaka kutolewa kwa azimio litakaloamua mipaka ya taifa la Palestina
ya baadaye kwa mujibu wa mipaka ya mwaka 1967.
Mwaka 1967, Israel iliyakalia maeneo ya Ukingo wa
Magharibi, Jerusalem Mashariki (al-Quds) na Ukanda wa Gaza lakini ikaondoka Gaza
na kisha kuizingira mwaka 2005.
Wapalestina wanataka kuundwa kwa taifa lao huru kwenye
maeneo ya Ukingo wa Magharibi, Jerusalem Mashariki ya al-Quds na Ukanda wa
Gaza.
0 comments:
Post a Comment