| Mahakama ya kijeshi nchini Nigeria (picha ya maktaba) |
Mahakama ya kijeshi nchini Nigeria imewahukumu askari 54
adhabu ya kifo kwa kukataa kupigana na wanamgambo wa kundi la Boko Haram huku
askari wengine watano wakiondolewa mashtaka.
Imeripotiwa kuwa askari waliotiwa hatiani walikataa
kushiriki operesheni ya kijeshi mwezi Agosti iliyolenga kuikomboa miji mitatu
inayoshikiliwa na Boko Haram.
Mwezi Septemba askari 12 walipewa adhabu ya kifo kwa
kile ambacho mahakama ilisema kuwa ni uasi na jaribio la kumuua kamanda wao wakati
wa operesheni ya kijeshi dhidi ya wanamgambo hao.
Kundi la Boko Haram limedai kuhusika na mashambulizi
kadhaa katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo tangu lilipoanzisha uasi wake
mwaka 2009. Mpaka sasa zaidi ya watu 10,000 wameshapoteza maisha katika
mashambulizi hayo.
Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumiwa
wakimbizi, Wanigeria wapatao 650,000 wameyakimbia makazi yao kutokana na
mashambulizi ya kundi hilo na wamegeuka kuwa wakimbizi wa ndani, huku maelfu ya
watu wakikimbilia katika mataifa jirani.
Kundi la Boko Haram – ambayo ina maana ya “elimu ya
Kimagharibi ni haramu” – linasema kuwa lengo lake ni kuiondosha madarakani
serikali ya Nigeria.
0 comments:
Post a Comment