| Rais Barack Obama wa Marekani |
Katika kile kinachoonekana kama mabadiliko makubwa ya
kisera, Rais wa Marekani Barack Obama ametangaza kuwa nchi yake na Cuba
zitarejesha uhusiano wa kideplomasia baada ya kuvunjika kwa zaidi ya miaka 50.
Akizungumza kutokea White House jana, Rais Obama alitangaza
kuhitimishwa kwa kile alichokiri kuwa ni sera “ngumu” ya kuitenga Cuba ambayo
haikuzaa matunda.
Rais Obama amesema kuwa ukurasa mpya umefunguliwa katika
uhusiano wa nchi hizo mbili na kwamba anataka kuwa na majadiliano ya dhati na
bunge la Congress kuhusu matarajio ya kuiondolea Cuba vikwazo vya kibiashara vilivyodumu
kwa kipindi cha nusu karne.
"Siamini kama tunaweza kuendelea kufanya mambo
yaleyale kwa zaidi ya miongo mitano halafu tukatarajia kupata matokeo tofauti. Vikwazo
havijasaidia”, alisema Rais Obama akizungumzia vikwazo vilivyowekwa dhidi ya
Cuba.
Aidha, Rais huyo wa Marekani alitangaza kuwa nchi yake
itafungua ubalozi mjini Havana, Cuba na kuongeza kiasi cha fedha ambacho
kinaweza kutumwa kutoka Marekani kwenda Cuba.
Alisema kuwa Washington itawezesha na kuidhinisha
miamala kati ya nchi hizo mbili, na kwamba upelekaji wa bidhaa kwenda Cuba
utarahisishwa zaidi kwa wafanyabiashara wa Kimarekani.
Tangazo hilo linakuja katika wakati ambako kumekuwa na
hali mpya ya hatua za kujenga uaminifu kati ya maadui hao wa muda mrefu, ikiwa
ni pamoja na kuachiliwa huru kwa mfungwa wa Kimarekani Alan Gross na kachero
mwingine, na pia kuachiliwa huru kwa Wacuba watatu waliofungwa Marekani.
Cuba na Marekani hazikuwa na uhusiano wa kidiplomasia
tangu mwaka 1961. Waligeuka kuwa maadui wakubwa muda mfupi baada ya mapinduzi
ya mwaka 1959 yaliyomuingiza madarakani Fidel Castro.
0 comments:
Post a Comment