| MWananchi akipita jirani na mti uliong'olewa na upepo mkali uliosababishwa na kimbunga Haiyan katika mji wa Cebu, katikati mwa Ufilipino, Novemba 8,2013. |
Na Kabuga Kanyegeri
KWA uchache, watu wapatao 10,000 wanahofiwa kupoteza
maisha katika jimbo la katikati mwa Ufilipino la Leyte baada ya kimbunga Haiyan
kuikumba nchi hiyo ya kusini mashariki mwa Asia.
Mkuu wa polisi katika jimbo hilo, Elmer Soria, ameseka
kuwa kimbunga hicho kiliharibu karibu asilimia 70 mpaka 80 ya eneo hilo wakati kikielekea
katika jimbo la Leyte.
Kimbunga Haiyan, ambacho kinasemekana kuwa kimbunga
machachari zaidi kuwahi kutokea Ufilipino, kiliangusha majumba, kikasababisha
mmomonyoko wa ardhi, mafuriko, kikakata umeme na mawasiliano katika visiwa sita
vya nchi hiyo.
Kimbunga hicho kilisababisha vifo vingi na hasara kubwa
kwenye kisiwa cha Leyte wakati kilipokuwa kikielekea katikati na kaskazini mwa nchi
ya Vietnam.
Maafisa nchini Vietnam wamewahamisha zaidi ya watu
500,000 kutoka katika maeneo yaliyotarajiwa kupitiwa na kimbunga hicho.
Wastani wa vimbunga 20 huipiga nchi ya Ufilipino kila
mwaka. Mwezi Desemba mwaka 2011, Kimbunga Washi kilisababisha vifo vya watu
1,200, kuwahamisha watu 300,000 na kuyaharibu zaidi ya makazi 10,000.
Mwaka jana kimbunga Bopha kilipiga katika miji mitatu ya
pwani kwenye kisiwa cha Mindanao, kikaua watu 1,100 na kusababisha uharibifu
unaokadiriwa kufikia Dola za Kimarekani bilioni 1.04.
Mwezi Septemba, Kimbunga Usagi, kilichokuwa kikisafiri
kwa kasi ya kilometa 240 kwa saa, kilipiga katika kisiwa cha Batanes kilichopo
kaskazini mwa nchi hiyo kabla ya kusababisha hasara kubwa nchini China.
0 comments:
Post a Comment