Na Kabuga Kanyegeri
RAIS wa Iran, Hassan
Rouhani amelielezea suala la urutubishaji wa madini ya urani ndani ya Iran kuwa
ni “msitari mwekundu” kwa nchi yake.
Rouhani ameyasema
hayo kufuatia mazungumzo baina ya Tehran na mataifa mataifa makubwa
yaliyofanyika hivi karibuni mjini Geneva.
“Kwetu sisi, mstari
mwekundu ni marufuku kwa mtu yeyote kuuvuka. Haki na maslahi ya Iran ni mstari
mwekundu kwetu; na haki hizo zinajumuisha haki za kuwa na nishati ya nyuklia
ndani ya utaratibu na sharia za kimataifa, na pia urutubishaji wa urani ndani
ya ardhi ya Iran,” alisema Rouhani wakati akilihutubia bunge la nchi hiyo leo.
Rouhani alifika
bungeni kumtetea mteule wake wa nafasi ya Wizara ya Vijana na Michezo, Nasrullah
Sajjadi. Kwa mujibu wa katiba ya Iran, mawaziri wanaoteuliwa na rais
wanalazimika kuhojiwa na kupitishwa na Bunge la nchi hiyo, Majlis.
Rais huyo wa Iran
alisisitiza kuwa “vikwazo, vitisho, hila na ubaguzi” havitakuwa suluhisho katika
kuamiliana na taifa lake.
“Jamhuri ya Kiislamu
ya Iran haijapiga magoti na haitapiga magoti mbele ya vitisho vyovyote,”
alisema.
Mapema leo, Iran na
mataifa matano yenye uanachama wa kudumu katika Baraza la Usalama la Umoja wa
Mataifa – Uingereza, Ufaransa, China na Marekani – pamoja na Ujerumani, walihitimisha
mazungumzo ya siku tatu juu ya programu ya nyuklia ya nchi hiyo.
Rouhani alitupilia
mbali madai kuwa vikwazo ilivyowekewa Tehran na Jumuiya ya Kimataifa
viliilazimisha kutaka suluhu na mataifa makubwa. Bali imekuwa ikifanya hivyo
tokea zamani, hata kabla ya vikwazo, kwa kuwa siku zote imekuwa muumini wa
utatuzi wa masuala mazito kwa njia ya mazungumzo badala ya vitisho.
Marekani, Israeli na
waitifaki wao wamekuwa wakiituhumu Iran kwamba inarutubisha madini ya urani kwa
ajili ya kutengeneza silaha za nyuklia, jambo lililoisukuma Marekani na Umoja
wa Ulaya kuiwekea vikwazo vya kiuchumi. Hata hivyo, Tehran imekuwa ikikanusha
madai hayo na kusema kuwa program yake inalenga kutumia teknolojia ya nyuklia
kwa miradi ya kijamii na ya amani.

0 comments:
Post a Comment