Na Kabuga Kanyegeri
Eneo la mashariki mwa Libya lenye utajiri wa mafuta
limeitangazia serikali yake, katika hatua ambayo inaweza kutafsiriwa kama
changamoto kwa serikali kuu ya taifa hilo la Kaskazini mwa Afrika.
Jana Jumapili, viongozi wa vuguvugu lililojitenga
walikutana katika mji wa Ajdabiya na kuizindua rasmi serikali yao chini ya jina
la Barqa au Cyrenaica. Katika sherehe hizo, zaidi ya mawaziri 20 walioneshwa
katika televisheni wakila kiapo.
Tangazo hilo ni pigo kwa serikali ya Tripoli ambayo
imekuwa ikijaribu kuzifungua upya bandari za eneo la mashari lenye utajiri
mkubwa wa mafuta ambazo zilifungwa kutokana na migogoro ya uasi na migogoro ya
kikabila, ambapo makundi hayo yanataka kupata fungu kubwa la madaraka na mapato
ya mafuta.
Aidha, hatua hiyo itazorotesha uhusiano kati ya
mashariki na Tripoli, ambayo imepinga vikali hatua hiyo.
Viongozi wa eneo la mashariki wanamtuhumu Waziri Mkuu wa
Libya, Ali Zeidan na baadhi ya wajumbe wa Baraza Kuu la Kitaifa kwa ufisadi na
kushindwa kuimarisha usalama tangu kuanguka kwa aliyekuwa rais wa nchi hiyo,
Kanali Muammar Gaddafi.
Uzalishaji wa mafuta nchini Libya umeshuka kwa asilimia
10 ya uwezo wake wa kuzalisha mapipa milioni 1.25 kwa siku kutokana na
maandamano na migomo kwa bandari na viwanda vya uzalishaji mafuta.
Eneo la mashariki limekuwa likikumbwa na matukio
mbalimbali ya ghasia na vurugu, ambapo askari mmoja aliuawa na mwingine
kujeruhiwa baada ya mgodi mmoja kulipuka jirani na kizuizi cha jeshi katika mji
wa Benghanzi juzi Jumamosi.
Katika tukio jingine, mlipuko wa bomu ulimuua afisa
upelelezi na binti yake katika mji huo.
Watu wapatao 100 walikusanyika katika mji huo kupinga
mauaji hayo wakiituhumu serikali ya Libya na bunge kwa kushindwa kuimarisha
usalama.
Tangu kuangushwa na kuuawa kwa Gaddafi mwaka 2011, serikali
ya Libya imekuwa ikikabiliana na uwepo wa wapiganaji wenye silaha, ambao
walishiriki katika mapambano dhidi ya utawala wa Gaddafi.
0 comments:
Post a Comment