Na Kabuga Kanyegeri
RAIS aliyeondolewa mdarakani nchini Misri, Muhammad
Mursi, leo amepelekwa mahakamani mashariki mwa mji mkuu wa nchi hiyo, Cairo,
kujibu mashitaka ya mauaji anayodaiwa kuyafanya katika kipindi cha uongozi wake
uliodumu kwa muda wa mwaka mmoja.
Mursi ambaye ni kiongozi wa kwanza kuchaguliwa
kidemokrasia nchini humo aliwasili leo kwenye mahakama iliyoko katika chuo cha
polisi.
Mursi anakabiliwa na mashitaka ya kuchochea ghasia na
mauaji yanayohusisna na vurugu zilizotokea nje ya ikulu mwezi Desemba 2012.
Iwapo atapatikana na hatia anaweza kuhukumiwa kifo au kifungo cha maisha
gerezani.
Maafisa kumi na nne wa Vuguvugu la Udugu wa Kiislamu,
wakiwemo wasaidizi watatu wa Mursi, nao watafika mahakamani leo.
Vuguvugu la Udugu wa Kiislamu limeyaelezea mashitaka
hayo kuwa yametengenezwa na kuwataka wafuasi wake kumiminika mitaani kupinga
hatua hiyo. Mpaka tunaandaa taarifa hii, mamia kwa maelfu ya wafuasi hao
wameitikia wito huo.
Muungano wa makundi yanayopinga mapinduzi ya kijeshi
yaliyomng’oa Mursi madarakani, umeeleza kuwa hautashirikiana na mamlaka za
serikali kwa sababu Mursi haitambui mamlaka ya mahakama hiyo.
Jana Jumapili, mamlaka zilibadilisha eneo la kuendeshea
kesi hizo kwa hofu ya kuibuka ghasia na umwagikaji wa damu. Uamuzi huo wa
dakika za mwisho ulifanyika baada ya wafuasi wa Mursi kuitisha maandamano
makubwa nje ya eneo la awali.
Mnamo Julai 3, mkuu wa jeshi la Misri, Jenerali Abdul
Fattah al-Sisi, alimuondoa Mursi madarakani. Baadaye rais huyo alikamatwa na
kupelekwa mahali kusikojulikana.
Mnamo Novemba 1, maelfu ya wananchi waliandamani nchi
nzima wakipinga mashitaka dhidi ya Mursi na kutaka arejeshwe madarakani. Aidha,
walitaka kuwajibishwa kwa wale waliohusika na mauaji ya wafuasi wa Mursi tangu
Julai 3.
Idadi kubwa ya maafisa na wafuasi wa Vuguvugu la Udugu
wa Kiislamu wanashikiliwa korokoroni.
Mashitaka hayo yanakuja muda mfupi baada ya ziara ya
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry, mjini Cairo. Kerry amekutana na
viongozi wakuu wa Misri, ambapo aliahidi Washington kuiunga mkono serikali ya
mpito ya nchi hiyo.

0 comments:
Post a Comment