![]() |
| Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk Richard Sezibera |
BAADA ya kimya juu ya mgogoro wa Jumuiya ya Afrika
Mashariki (EAC), hatimaye Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo, Dk Richard Sezibera,
ameibuka na kusema kuwa mgogoro miongoni mwa nchi wanachama utajadiliwa kwa
kina katika kikao kijacho cha Baraza la Mawaziri.
Kikao hicho cha mawaziri, kwa mujibu wa Dk Sezibera,
kitafanyika Novemba 28 mwaka huu. Kikao hicho ndicho kikao cha juu ambacho
kinatoa mapendekezo mbalimbali yanayoenda kujadiliwa kwenye vikao vya wakuu wa
nchi wanachama.
Dk Sezibera ambaye ni raia wa Rwanda, ndiye anayeongoza
Sektarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki yenye makao yake makuu mjini Arusha
na alikuwa hajasema lolote tangu kuanza utaratibu wa nchi tatu kukutana bila
kushirikisha Tanzania na Burundi na wala haijajibu malalamiko ya Serikali ya
Tanzania.
Katika taarifa yake, Katibu Mkuu huyo alikiri kupokea
malalamiko kutoka kwa nchi za Burundi na Tanzania kuhusu wasiwasi wa vikao
kadhaa vilivyofanywa na viongozi wakuu wa nchi za Kenya, Rwanda na Uganda bila
kuwashirikisha wanachama wenzao.
Kwa muda sasa muungano huo haramu wa nchi tatu umekuwa
unaripotiwa kwa kina na vyombo vya habari kuhusu kutengwa kwa nchi hizo mbili,
lakini sektarieti hiyo iliendelea kukaa kimya.
Tanzania ilitoa tamko la wazi kuwa nchi hizo zimekiuka
makubaliano yaliyoko kwenye mkataba wa jumuiya hiyo.
“Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ameshauriana
na nchi tano wanachama kuhusu suala hilo,” alisema Dk Sezibera na kuongeza kuwa
katika mkutano wa 19 wa Baraza la Mawaziri wa kisekta, alibadilishana mawazo na
mawaziri na wote walionesha nia ya kuendelea kujenga jumuiya hiyo, ikiwa ni
pamoja na kushughulikia changamoto zilijitokeza.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, Katibu Mkuu
huyo amewaomba wananchi wa Afrika Mashariki wasishtushwe na changamoto
zilizojitokea, kwani zinashughulikiwa na zitajadiliwa kwa kina katika mkutano
wa mawaziri ambao utafanyika Novemba 28 na utatoa mapendekezo juu ya
kilichojiri kwenye mkutano huo.
Alisema nchi wanachama zimedhamiria kuanza utekelezaji
wa itifaki za soko la pamoja na ushuru wa forodha, ikiwa ni pamoja na
uimarishaji wa miundombinu, kuondoa vikwazo kwenye usafirishaji wa mizigo ya
biashara, huduma na watu.
Rais Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda na
Uhuru Kenyatta wa Kenya juzi walikutana tena mjini Kigali, Rwanda, pamoja na
mambo mengine, walitarajia kusaini makubaliano ya kuanzisha kituo kimoja cha
kukusanya ushuru kinachotarajia kurahisisha uchukuzi wa bidhaa kutoka Mombasa
nchini Kwenya, Uganda hadi Rwanda.
Katika mkutano huo, Rais Salva Kiir wa Sudan alialikwa
kama mshirika. Mkutano huo ulifanyika baada ya ule uliofanyika mjini Kampala
Uganda, Juni mwaka huu na mwingine uliofanyika Mombasa, Agosti, ambako viongozi
hao watatu walipendekeza kupanuliwa kwa Bandari ya Mombasa, ili kuwezesha
uharaka wa bidhaa kupitishwa katika kuhudumia Kanda nzima.
Hivi karibuni, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Samuel Sitta, alitangaza kuwa Tanzania itatoa ‘talaka’ kwa nchi za
Rwanda, Kenya na Uganda ambazo zimeamua kuanzisha Jumuiya ya hiari nje ya
Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Sitta alisema kutokana na nchi hizo kuonekana kuitenga
Tanzania na Burundi ambazo ni wanachama wa jumuiya hiyo, wameshaanza mazungumzo
ya kushirikiana kiuchumi, kisiasa na nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia
ya Watu wa Congo (DRC).
“Hawa wenzetu wanafanya utoto wa kutuzunguka, sisi
tunatumia hekma za mzee Mwinyi alieyesema ‘mwongo, mwongoze’. Kama wao wana
hila zozote juu yetu, siku si nyingi tutazibaini, kama ndoa kwenye jumuiya basi
sisi ndio tutakuwa tumeoa… hivyo tutatoa talaka wakati wowote,” alisema Sitta
baada ya kutakiwa kutoa ufafanuzi na Wabunge.

0 comments:
Post a Comment