POLISI: ZANZIBAR KUNA MGOGORO





JESHI la Polisi visiwani Zanzibar, limesema ndani ya jamii ya Wazanzibari kuna mgogoro uliojificha unaosababisha kuwepo kwa matukio yenye sura ya kigaidi. Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar, Mkadam Khamis Mkadam, ndiye aliyefichua ukweli huo katika mahojiano yake na MTANZANIA Jumatano jana kupitia simu yake ya kiganjani.


Kamanda Mkadam ambaye alikuwa akizungumzia uchunguzi wa awali wa Jeshi la Polisi kuhusu mlipuko wa bomu lililorushwa dukani katika eneo la Darajani Makontena, alisema taarifa za awali za kikachero zimeonyesha kuwa upo mgogoro uliojificha miongoni mwa watu wa jamii ya Zanzibar unaosababisha kuwapo kwa matukio ya kihalifu.

Kamanda huyo alisema, watu waliokuwa katika gari aina ya Pick Up, walirusha bomu hilo lililokuwa na muundo wa Soseji katika duka la Sahara Store linalomilikiwa na mfanyabiashara aliyemtaja kwa jina moja la Himid.

Alisema tukio hilo lilitokea siku ya Jumapili majira ya saa 8:30 mchana.

Kamanda Mkadam alisema bomu hilo halikuweza kuharibu duka hilo, badala yake liliangukia sanduku zenye chupa za soda ambapo mmoja wa walinzi aliyekuwapo eneo hilo, Amour Kassim, alilichukua na kulitupa.

Taarifa za kikachero zimemnukuu mlinzi huyo akieleza kuwa aliuchukua mfuko uiliorushwa na watu waliokuwa kwenye Pick up, lakini alibaini kuwa unatoa moshi mwingi ndipo aliurusha barabarani na kutoa kishindo kikubwa ambacho kilichimba barabara.

Awali Kamanda Mkadam alisema kitu kitakachoweza kusaidia uchunguzi wa Jeshi la Polisi ni masalia ya unga mweupe na kokoto zilizochimbika na kuwataka wananchi kuwa watulivu wakati vyombo vya usalama vikiendelea kufanya uchunguzi.

Kamanda Mkadam alisema taarifa za awali za polisi zimeonyesha yapo makundi ya watu Zanzibar walioamua kutendeana visa, ikiwa ni pamoja na tukio la kurushwa bomu eneo la darajani eneo la maduka, pamoja na matukio ya watu kushambuliwa kwa tindikali.

“Tunatafuta taarifa za makundi yanayofanyishiana, upo mgogoro mkubwa kati ya watu na watu au makundi kwa makundi, hizi ni taarifa za awali za kipolisi kwamba kuna mgogoro umejificha.

“Kuna uhalifu uliojificha na tumeanza kupata taarifa zake na tutawaeleza hivi karibuni, kwa sasa ni mapema mno kuueleza umma,” alisema Mkadam.

Kamanda Mkadam alisema polisi inaendelea kufanya kazi yake ya upelelezi kwa uhakika juu ya tukio la kurushwa bomu la mkono na yale ya watu kushambuliwa kwa tindikali, ili wasipotoshe ushahidi.


“Tumehoji watu wengi na bado hatujakamata, tunafanya kazi yetu kwa uhakika ili tuwe karibu na taarifa zetu, tunajitahidi kutafuta habari,” alisema.


CHANZO: Mtanzania
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 comments:

Post a Comment