| Wanamgambo wa Boko Haram |
Kundi la Boko Haram la nchini Nigeria linadaiwa kuwateka
watu 185 katika kijiji cha Gumsuri kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka nchini humo leo, kundi hilo
lilifanya shambulizi katika kijiji hicho lililowaua watu wasiopungua 33 na
kuwateka wengine 185.
Shambulizi hilo linadaiwa kutokea Desemba 14; hata hivyo
habari za tukio hilo zimetolewa leo baada ya manusura wa shambulizi hilo baya
kufanikiwa kufika katika mji wa Maiduguri.
Maofisa katika eneo hilo wanasema kuwa mateka walibebwa
kwenye magari ya wazi na kupelekwa katika msitu wa Sambisa, ngome ya kundi
hilo.
Wakati huo huo, duru za kijeshi kutoka nchini Cameroon, jirani
na eneo la mashariki mwa Nigeria, zinasema kuwa wanamgambo 116 wa kundi hilo wameuawa wakati wa mapambano na jeshi la Cameroon.
Mnamo Aprili 14, kundi la Boko Haram liliwateka
wanafunzi wa kike 276 kutoka shule moja ya sekondari katika mji wa Chibok
kaskazini mwa nchi hiyo.
Tukio hilo liliibua kelele kutoka kila kona ya dunia. Utawala
wa Nigeria umekuwa ukikosolewa vikali kwa kushindwa kuzima ghasia zinazolikumba
taifa hilo.
Kundi la Boko Haram – ambayo ina maana ya “elimu ya
Kimagharibi ni haramu” – linasema kuwa lengo lake ni kuiondosha madarakani
serikali ya Nigeria.
Kundi hilo limedai kuhusika na mashambulizi kadhaa
katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo tangu lilipoanzisha uasi wake mwaka 2009.
Mpaka sasa zaidi ya watu 10,000 wameshapoteza maisha katika mashambulizi hayo.
Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumiwa
wakimbizi, Wanigeria wapatao 650,000 wameyakimbia makazi yao kutokana na
mashambulizi ya kundi hilo na wamegeuka kuwa wakimbizi wa ndani, huku maelfu ya
watu wakikimbilia katika mataifa jirani.
0 comments:
Post a Comment