Na Kabuga Kanyegeri
WATU kumi na tatu wamepoteza maisha katika ghasia
zinazohusiana na madawa ya kulevya katika mji wa kaskazini mashariki wa
Matamoros nchini Mexico.
Matukio matatu tofauti ya kushambuliana yametokea leo
Jumapili katika mji huo wa kaskazini mwa jimbo la Tamaulipas.
Kwa mujibu wa taarifa ya serikali ya jimbo, matukio
mawili yalitokea baina ya majambazi na vikosi vya usalama vya Mexico. Watu 8
wamepoteza maisha katika mapambano hayo.
Aidha, wanaume wanne na mwanamke mmoja walipigwa risasi
na kufa hapo hapo katika mapambano yaliyotokea mapema leo baina ya makundi
ambayo hayakutambuliwa.
Jimbo la Tamaulipas limepata umaarufu wa kuwa miongoni
mwa majimbo yenye ghasia na uhalifu wa kutisha nchini Mexico.
Katika miaka ya hivi karibuni, magenge ya madawa ya
kulevya yanayofanya biashara hiyo katika jimbo hilo yamefanya matukio kadhaa ya
mauaji, mapambano ya silaha na utekaji wakati yakiwania udhibiti wa njia ya
biashara hiyo kuelekea Marekani.
Hii ni changamoto nyingine kwa Rais Enrique Nieto, aliyeingia
madarakani mwezi Desemba mwaka jana, ambapo aliahidi kukomesha ghasia za
magenge hayo ambazo zimegharimu maisha ya watu wapatao 80,000 tangu mwanzoni
mwa mwaka 2007.
Takwimu rasmi zinaonesha kuwa tangu Nieto aingie
madarakani, kila mwezi watu 1,000 hupoteza maisha katika matukio yanayohusisha
biashara ya madawa ya kulevya na jeshi la Mexico linaendelea kupambana na
magenge hayo katika maeneo mengi ya nchi hiyo.
Mapema mwaka huu, Nieto alikiri kuwa mtandao wa magenge
ya kihalifu una nguvu kubwa na yana udhibiti katika maeneo kadhaa ya nchi,
ikiwa ni pamoja na majimbo ya Michoacan,
Mexico na Guerrero, licha ya kuongezwa kwa idadi ya wanajeshi katika maeneo
hayo.
0 comments:
Post a Comment