Na Kabuga Kanyegeri
MAHAKAMA nchini Misri imeakhirisha kesi inayomkabili
rais wa kwanza kuchaguliwa kidemkrasia nchini humo, Muhammad Mursi, huku
wafuasi wake wakiandamana nje ya mahakama.
Ikiwa ni mara ya kwanza kuonekana hadharani baada ya
kupinduliwa na jeshi miezi minne iliyopita, Mursi alifikishwa leo kwenye
mahakama hiyo iliyoko katika chuo cha mafunzo ya polisi.
Kesi ya msingi ilisimamishwa mara tu baada ya kuanza.
Kesi dhidi ya Mursi na washitakiwa wenzake imepangwa kuendelea Januari 8.
Uamuzi huo ulikuja baada ya washitakiwa kuanza kupaza
sauti za kulipinga jeshi, wakisema kuwa hawayatambui mamlaka ya mahakama.
Mursi anaripotiwa kusema kuwa yeye ndiye rais halali wa
Misri na kuitaka mahakama iache mara moja kile alichokiita kuwa ni idhilali kwa
rais halali.
"Mimi ni Dk Muhammad Mursi, rais wa jamhuri… Hii
mahakama ni batili,” Mursi alisema wakati kesi ikianza na kuongeza, “Haya
yalikuwa mapinduzi ya kijeshi. Viongozi wa mapinduzi haya wanatakiwa
kushitakiwa. Mapinduzi ni uhaini na ni jinai.”
Mursi, na wanachama 14 wa Vuguvugu la Udugu wa Kiislamu
wanatuhumiwa kuchochea ghasia zilizosababisha kuuawa kwa watu 10. Vuguvugu hilo
limeyaita mashitaka hayo kuwa ya kutengenezwa.
Kwa sasa usalama umeimarishwa nchini Misri huku kiasi
cha polisi 20,000 wakitumika kudumisha usalama katika mitaa mbalimbali.
Wafuasi wa vuguvugu la Udugu wa Kiislamu wameandamana
katika miji kadhaa na nje ya mahakama. Ripoti zinasema kuwa mamia ya
waandamanaji wamekamatwa.
Mapema Ijumaa, maelfu ya watu waliingia mitaani nchi
nzima kupinga mashitaka dhidi ya Mursi na kutaka kiongozi huyo arejeshwe
madarakani.
Aidha, walitaka haki itendeke kwa wafuasi wenzao
waliouawa katika operesheni ya jeshi dhidi yao baada ya kuondolewa kwa Mursi.
Idadi kubwa ya maafisa na wafuasi wa chama hicho
wameshikiliwa na jeshi na vikosi vya polisi tangu miezi kadhaa sasa, huku mamia
ya wafuasi wengine wakiuawa katika operesheni ya vikosi vya usalama dhidi yao.
0 comments:
Post a Comment